Katika uandishi watu huweza kutofautiana katika namna ya uandikaji wa maneno, hili huweza kutokea kutokana na sababu mbalimbali. Kwa upande mwingine yapo maneno ambayo aghalabu waandishi wengi huwa tunayakosea kuyaandika.
 
Yafuatayo ni baadhi ya maneno ambayo hayakupaswa kuandikwa hivyo kwa mujibu wa kanuni ya maumbo ya maneno.
Maneno hayo ni Muamuzi, alimwuliza, muachia, mwuwaji, muelekeo, hakumueleza, walimuangalia, alimuona, muislamu, muafaka, muongo, mwumbaji, muendesha n.k
 
Kikanuni ‘Mu’ iliyo katika neno itabadilika na kuwa ‘Mw’ iwapo itafuatiwa na irabu zifuatazo; ‘a’, ‘e’, ‘i’ na ‘o’
Yaani;
 
1. Mua… = Mwa…
(‘Mua’muzi = mwamuzi, ‘mua’faka = mwafaka, wame’mua’chia = wamemwachia, ‘mua’limu = mwalimu, ali’mua’ngalia= alimwangalia)
 
2. Mue… = Mwe…
(‘Mue’ndelezo = mwendelezo, ali’mue’lewesha = alimwelewesha, haku’mue’lewa = hakumwelewa, aka’mue’lewesha= akamwelewesha, haku’mue’leza= hakumweleza)
 
3. Mui… = Mwi…
(‘Mui’slamu = ‘Mwi’slamu, wali’mui’ngiza = walimwingiza, ali’mui’ta = alimwita, yaka’mui’shia = yakamwishia, ‘mui’gizaji = mwigizaji)
 
4. Muo… = Mwo…
(‘Muo’ngozo = mwongozo, ali’muo’na= alimwona, wali’muo’nesha = walimwonesha, ata’muo’ndolea = ata’mwo’ndolea, nime’muo’ngopea= nimemwongopea)
Sababu kuu ya mabadiliko hayo imetokana na jinsi tunavyoyatamka maneno hayo (mfano; muongozo, alimueleza, mualimu). Ukichunguza vizuri unavyoyatamka maneno haya utabaini kuwa kuna ‘w’ inayojitokeza (kwenye matamshi), pindi ‘Mu’ inapokutana na irabu a, e, i & o.
Hii ndiyo sababu ya mwonekano wa maneno; Mwafaka, walimweleza, Mwislamu, tunamwongozo, alimwona, walimwelekeza n.k
 
5. Muu… = Muu…
Kama umefuatilia vizuri utabaini kuwa Muu… haipokei mabadiliko, ‘Mu’ inapokutana na irabu ‘u’ hakuna mabadiliko yanayotokea, neno hubaki kama lilivyokuwa; Alimuuliza, muuguzi, Muumba, muungano, muuaji, muujiza n.k
 
Angalizo.
Katika mazingira ambayo neno litabadilika maana (baada ya kubadilika kutoka MU kwenda MW), neno hilo litaachwa kwenye asili yake.
Mfano 1;
Neno ‘alimuaga’ huwezi kulibadilisha na kuwa ‘alimwaga’ sababu neno ‘alimwaga’ lina maana nyingine, hivyo neno ‘alimuaga’ litabaki kama lilivyo